Faida ya Safaricom yafika $381m
Kampuni ya mawasiliano ya Safaricom
nchini Kenya imetangaza ongezeko la asilimia 19.6 katika faida yake ya
mwaka wa kifedha uliomalizika Machi mwaka huu baada ya kutozwa kodi,
ikisaidiwa sana na ukuaji wa mapato kutoka kwa M-Pesa na data.
Mapato kutoka kwa M-Pesa yaliongezeka asilimia 27.2 na kufikia Sh41.5 bilioni ($415 milioni) katika kipindi hicho huku idadi ya wateja wanaotumia huduma hiyo na kutuma na kupokea pesa angalau siku moja kwa mwezi ikipanda asilimia 17.5 hadi 16.6 milioni.
Jumla ya thamani ya shughuli za kibiashara zilizofanywa kupitia M-Pesa ilipanda asilimia 27 hadi Sh5.29 trilioni ($52.9 bilioni).
Mapato kutoka kwa data yalikua asilimia 42.7 na kufikia Sh21.2 bilioni ($212 milioni), wateja wanaotumia data kupitia simu zao angalau mara moja kwa mwezi wakiongezeka asilimia 21.5 hadi 14.1 milioni.
Kufikia Desemba mwaka 2015, Safaricom ilikuwa ikiongoza kwa kuwa na wateja wengi nchini Kenya, ikiwa na asilimia 64.7 ya wateja wote. Idadi hiyo hata hivyo ilikuwa imeshuka kutoka asilimia 67 jambo ambalo kampuni hiyo inasema lilitokana na kubadilishwa kwa mfumo wa kuhesabu wateja.

Maoni
Chapisha Maoni