Ni miaka 3 tangu alipofariki rapper Albert Mangwair (1982-2013)
Leo imetimia miaka mitatu tangu rapper Albert Mangwair alipo afariki dunia nchini Afrika Kusini.
Albert Mangwair maarufu kama Ngwair alifariki tarehe 28 Mei 2013 nchini Afrika Kusini ambako alikwenda kwa ajili ya shughuli zake za muziki.
Habari kuhusu kifo cha Ngwair zilianza kusambaa kwenye mitandao ya kijamii kwa kasi sana kitu kilichowashtua watu wengi sana. Zilikuwa kama uvumi tu na wengi waliamini ni utani ambao baadaye ungeisha lakini ikaja kubainika kuwa ni habari ya kweli. Nchini Afrika Kusini Ngwair alikuwa na rafiki yake M TO THE P waliopelekwa kwenye hospitali ya St Helen ya jijini Johannesburg wakiwa mahututi na haikufahamika kwa uhakika kabisa ni nini kiliwapata.
Habari zilivuma kuwa Ngwair amefariki kutokana na kutumia kiasi kikubwa cha dawa za kulevya. Tuhuma hizi hadi leo hazithibitishwa kama ndicho kitu kilichochukua uhai wa rapper huyo. Marafiki zake wa karibu waliokuwa naye muda mwingi walieleza kuwa kuwa mpaka anapelekwa hospitali alikuwa hajitambui na huenda alifariki akiwa usingizini.
Ngwair alikuwa ni moja kati ya rappers hatari sana kuanzi kwenye freestyle hadi kwenye mziki wake. Kutokana na umaarufu wake aliokuwa nao, taarifa za kifo chake ziliihuzunisha sana Tanzania kwani ni kweli tulipoteza jembe.
Akizungumza na kituo kimoja cha television, TID ambaye alikuwa rafiki wa karibu na Ngwair alisema kuwa anasikitikana sana kumpoteza aliyekuwa rafiki yake kipenzi kwani walikua pamoja na walisaidiana karibia kwenye kila jambo. Aidha TID alitaka yeyote mwenye hati miliki ya nyimbo za marehemu Ngwair, azikazidhi kwa mama yake mzazi ili na mama naye afaidi matunda ya mwanae.
Aidha wasanii nao walieleza hisia zao juu ya kifo cha Ngwair. Profesa Jay alikaririwa akisema “inaniuma sana lakini sina cha kufanya kwa kuwa ni kazi ya Mungu na kazi yake haina makosa, kinachotakiwa ni kumuombea apumzike kwa amani huko aendako.”
“Sidhani kama atanitoka kichwani kwangu, naona kama ametutoroka kwa kuwa hatuhitaji aondoke muda huu lakini hakuna jinsi tutakutana naye siku ya mwisho na nitamweleza machungu yangu na kwa jinsi gani kifo chake kimeniumiza,” alisema Afande Sele.
Albert Keneth Mangwair alizaliwa tarehe 16 Novemba 1982 Mbeya, Tanzania. Baada ya muda familia yake ilihamia ambapo yamekuwa makazi yao ya kudumu na alifariki tarehe 28 Mei 2013 akiwa na umri wa miaka 31.
Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi, Amina.
Maoni
Chapisha Maoni