BAADA KUMKOSA VARDY WENGER BADO YUPO LEICESTER, AMLENGA KANTE!
BAADA ya kumkosa Jamie Vardy ambae amethibitishwa kubakia na Mabingwa wa England Leicester City, Meneja wa Arsenal Arsene Wenger hajabanduka kwa Mabingwa hao na sasa ameelekeza nguvu zake kwa Kiungo N'Golo Kante.
Jana Leicester ilitoa tamko rasmi kwamba Straika huyo ambae sasa yuko France akiichezea England EURO 2016 atabakia Klabuni kwake.
Mapema Mwezi huu, Arsenal iliivamia Leicester na kutoa Ofa ya Pauni Milioni 20 ambayo ndiyo imo kwenye Mkataba wa Vardy akitakiwa na Klabu nyingine na kila dalili zilikuwepo kwamba atahamia Emirates.
Lakini Vardy mwenyewe akasita kutoa uamuzi wa haraka na Wiki iliyopita Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger, akanyoosha Mikono juu na kuungama kuwa Straika huyo aliefunga Bao 24 na kuipa Ubingwa Leicester atabakia Leicester.
Mara baada ya uthibitisho huo kuhusu Vardy, Arsene Wenger sasa amedokeza nia ya Arsenal kumsaini Kiungo N'Golo Kante Mchezaji mwenzake Vardy huko Leicester City.
Hivi sasa Kante yuko na France akiicheza kwenye EURO 2016 ambako anawika kama alivyofanya akiisaidia Leicester kutwaa Ubingwa wa England Msimu uliokwisha juu ambao ulikuwa Msimu wake wa kwanza Klabuni hapo.
Kitu kinachompa Imani Wenger kwamba Kante wanaweza kumpata ni hatua ya Leicester ya kujitayarisha kwa kumnunua mbadala wa Kante, mwenye Miaka 25, ambae ni Kiungo toka Klabu ya France Nice aitwae Nampalys Mendy.
Licha ya tayari kumnasa Kiungo wa Uswisi Granit Xhaka, Wenger ameeleza: “Ni ngumu kuelezea hili kwa sasa. Kante yupo kwenye Listi ya Klabu nyingi. Na ni eneo ambao tuna Wachezaji wengi. Lakini tutaona nini kinatokea katika Wiki mbili au tatu zijazo. Inaonekana Leicester wamenunua Mchezaji kutoka Nice Nampalys Mendy ambae yupo kama Kante na hilo inaelekea wanajitayarisha kumpoteza Kante, hatujui!”
Wenger alimaliza: “Ukiwauliza Watu 100 Mtaani kama wanataka Kante kuichezea France utapata majibu 100 ya ndio. Amefanya kazi njema katika Gemu mbili na sishangai!”

Maoni
Chapisha Maoni