Sare ya 1-1, dhidi ya Zanaco, imewaweka katika wakati mgumu wa kucheza hatua ya makundi Yanga ya michuano hiyo mikubwa Afrika.
Sare hiyo imeonekana kuwamuza mashabiki wa timu hiyo kufuatia kiwango kibovu, kilichoonyeshwa na timu yao jambo lililowalazimu kumfuata kocha wao wa zamani Mdachi Hans van der Pluijm na kumwomba arudi kuifundisha timu hiyo.
Matokeo yanamaanisha Yanga watahitaji ushindi wa ugenini katika mchezo wa marudiano nchini Zambia ili kuingia hatua ya makundi ya michuano hiyo.
Yanga iliyokuwa nyumbani leo ilionyesha kiwango dhaifu na kuwaacha wageni weo wakijitawala na kufanya anavyotaka ikiwapo kupoteza nafasi nyingi za mabao.
Katika mchezo huo uliochezeshwa na marefa kutoka Djibouti, Djamal Aden Abdi aliyeyesaidiwa na Hassan Yacin na Farhan Salime, hadi mapumziko Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0.
Yanga pamoja kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa bao moja lililofungwa na Simon Msuva dakika ya 39, lakini muda mrefu walionekana kuhangaika uwanjani kutafuta mpira uliokuwa miguuni mwa wachezaji wa Zanaco.
Bao hilo lilifungwa na winga machachari wa timu hiyo, Simon Happygod Msuva dakika ya 39 baada ya kuwachambua mabeki wa Zanaco kufuatia pasi nzuri ya kiungo Mzambia, Justin Zulu.
Bao hilo lilikuja baada ya Yanga kubadilisha maarifa ya kuwashambulia Zanaco, kutoka kutumia mipira ya kutokea pembeni hadi kuamua kuingia ndani ya eneo la hatari kwa kugongeana pasi.
Kwa dakika zote 30 za awali, Zanaco hawakuwa na kazi ngumu kudhibiti mashambulizi yatokeayo pembeni ya Yanga, lakini baada ya mabingwa wa Tanzania, kubadilika hali ikawa ngumu upande wake.
Pamoja na kufunga bao moja, lakini ndani ya dakika 15 za kuelekea mwisho wa kipindi cha kwanza, Yanga walikosa mabao mawili zaidi ya wazi.
Kipindi cha pili Zanaco walikuja na maarifa mapya na kufanikiwa kuziba mianya ya Yanga kupenyezeana pasi hivyo kupunguza kasi ya wawakilishi hao wa Tanzania.
Yanga ikarudi kutumia mipira mirefu ya kutokea pembezoni mwa Uwanja kujaribu kulazimisha mashambulizi langoni mwa Zanaco, lakini safu ya ulinzi ya mabingwa hao wa Zambia ilikuwa imara.
Hatimaye Zanaco wakafanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 78 kupitia kwa mshambuliaji wake Mghana, Attram Kwame aliyetumia mwanya wa mabeki wa Yanga kuzubaa kusubiri wapinzani wao watoe nje mpira kiungwana baada ya mchezaji mwenzao, Obrey Chirwa kuangushwa.
Kwame alifunga mbele ya mabeki wa kati watatu wa Yanga Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan na Vincent Bossou na kipa wao Deogratius Munishi ‘Dida’ baada ya krosi kutoka wingi ya kulia.
Bao hilo lilionekana kabisa kuwavunja nguvu Yanga na kutoka hapo wakaanza kucheza ili kumalizia mchezo kwa sare na si kutafuta ushindi.
Wachezaji Juma Mahadhi na Emmanuel Martyin walioingia kwa upande wa Yanga kuchukua nafasi ya Donald Ngoma na Thabani Kamusoko, walionekana kushindwa kuiunganisha timu na kuzidi kuwapa nguvu wapinzani wao Zanaco kuendelea kuwashambulia.
Matokeo hayo yanawalazimu Yanga kushinda mchezo wa marudiano ili waweze kufuzu hatua ya makundi vinginevyo huo utakuwa ndiyo mwisho wao na ndoto za kuutwa ubingwa wa michuano hiyo kwa mwaka huu licha ya kumchukua kocha Lwandamina aliyeifikisha Zesco ya Zambia nusu fainali ya michuano hiyo mwaka jana.
Maoni
Chapisha Maoni